INEOS 1:59 Challenge: Eliud Kipchoge aushinda mkono wa muda!

Muktasari:

Vienna ipo mita 150, kutoka usawa wa bahari, wakati ambapo Eldoret, ambapo ndipo ilipo ambi yake ya mazoezi ni mita 2000 kutoka usawa wa 2000. Maana yake ni kwamba, hali ya hewa ya Eldoret, ilisaidia sana kufanikisha ushindi wa Kipchoge.

KWA macho ya kawaida ya binadamu wa kawaida, mbio za IEOS 1:59 Challenge, si mbio ya kawaida kama ilivyo mbio nyingine. Asikudanganye mtu! Kukimbia kilomita 42 ndani ya muda huo,sio rahisi hata kidogo!
Bingwa wa Dunia wa Marathon na mshikilizi wa rekodi, Eliud Kipchoge, ambaye ni mzaliwa wa Kapsisiywa, kaunti ya Nandi, eneo la Bonde la ufa, nchini Kenya, aliuonesha ulimwengu mzima ukomo wa uwezo wa Mwana wa Adamu.
Achana na kampeni iliyofanyika dunia nzima kuhamasisha mbio hizo zisizotambulika na Shirikisho la Riadha Duniani. Sahau kabisa kuhusu pesa zilizomwagwa kudhamini mbio hizi. Sahau pia kuhusu furaha iliyoko kwenye mioyo ya Wakenya na Waafrika.
Tangu kuumbwa kwa Dunia, tulishuhudia mwanadamu akipambana na mkono wa sekundu wa saa. Jiji zima la Vienna ilisimama. Dunia nayo ikakataa kuzunguka kwa muda. ‘INEOS 1:59 Challenge’ na Kipchoge kwa kweli wametuonesha ‘No Human is Limited’
Akiongozwa na wakimbiaji ‘Pace Makers’ 41, kutoka mataifa zaidi ya 20 tofauti, bingwa huyu wa Olimpiki, alianza kukata mawimbi ya ardhi, akisaidiwa na kiatu cha kipekee kilichotenengezwa maalum (Nike ZoomX Vaporfly NEXT%), kwa ajili ya mbio hizo na Kampuni ya Nike, akikimbia nyuma ya gari maalum.
Akishindana na rekodi yake, Kipchonge alianza kampeni hiyo, taratibu kuanzia saa 3:15 asubuhi, kwa saa za Afrika Mashariki (saa moja na dakika 15 kwa saa za Austria). Kwa kasi ile ile, kilomita 20 zilimalizika ndani ya dakika 57. Dunia inashangaa?
Hadi kufikia saa 4:44 asubuhi, tayari Kipchoge alikuwa amekamilisha kilomita 31, ambapo kwa mujibu wa mkono wa muda, zilimchukua saa 1:28:03 kumaliza kilomita na kubakisha kilomita 11 tu kuweka rekodi itakayotikisa Dunia. Alihitaji dakika 28 kujishangaa!
Saa tano kamili asubuhi, zilimkuta Kipchoge akimaliza kilomita 34, akiwa ametumia saa 1:40:34 na kubakisha kilomita sita, ambazo ni sawa na dakika 19, kuweka rekodi mpya. Kufika saa 5:10 tayari alikuwa amemaliza kilomita 39, akitumia muda wa 1:52:04 ambapo zilibaki kilomita 2.6 kukamilisha mbio.
REKODI
Hatimaye! Lile ambalo wengi walidhani lisingewezakana liliwezekana ndani ya Jiji la Vienna. Historia iliandikwa baada ya muda wa saa 1:59:40. Dunia itamkumbuka mwana Kipchoge  aliyeushangaza ulimwengu kwa kuushinda mkono wa muda! Haijawahi kutokea!
Akiongozwa na timu namba 9 ya waongoza mbio “ambayo iliundwa na Wakenya watatu, Bingwa wa Dunia na mshikilizi wa rekodi ya Marathon na ubingwa wa Olimpiki, alivuka utepe sekunde 9 mbele ya muda uliowekwa. ‘Parte after Parte’
ZAWADI
Kukamilisha mbio hizo ndani ya muda huo maana yake nini? Maana ni kwamba, Kipchoge ndio mwanaume mwenye kasi zaidi duniani, kwenye mbio za Marathon, zimemuongezea Kipchoge Ksh 400 milioni sawa na Sh 8.9 Bilioni za Kitanzania, kwenye akaunti yake.
Mbali na pesa hizo, Kampuni ya magari ya Isuzu, itamzawadi gari mpya aina ya Isuzu, Double Cabin, lakini pia wadhamini wa mbio hizo, hawajasema ni kitu kitafuata baada ya ushindi huo.
KIPCHONGE ANASEMAJE?
Baada ya kumaliza mbio hizo, alipoulizwa anajisikiaje, Kipchoge hakusita kumshukuru Mwenyezi Mungu huku akisisitiza kwamba, kama kuna siku aliwahi kuwa katika wakati mgumu ni dakika chache kabla ya saa 3:15 (2:15 saa za Vienna).
“Nashukuru Mungu kwa kufanikisha ndoto hii, kama nilivyosema awali, hakuna binadamu asiyeweza kufanya maajabu, kila mtu ana uwezo wa kufanya atakalo akijiamini….kabla ya saa mbili na robo, nilikuwa katika wakati mgumu sana, nadhani nilikuwa na mchecheto,” alisema Kipchoge
UGUMU WA NJIA
Vienna ipo mita 150, kutoka usawa wa bahari, wakati ambapo Eldoret, ambapo ndipo ilipo ambi yake ya mazoezi ni mita 2000 kutoka usawa wa 2000. Maana yake ni kwamba, hali ya hewa ya Eldoret, ilisaidia sana kufanikisha ushindi wa Kipchoge.
Mbali na hali ya Kijiografia ya Vienna, waandaaji ambao ni Ineos, Kampuni ya Nike na Sir Ratcliffe, walihakikisha wanachagua njia yenye barabara tatu tofauti, ambayo ingemsaidia kumkinga na dhoruba ya upepo (wind drag).
Njia hiyo ilinyooka kwa asilimia 90. Hiyo inamsaidia kukimbia kwa kasi zaidi. Kongole kwa mwana wa adamu Kipchoge. Kwa mara ya kwanza, mwanadamu ameushinda mkono wa muda. Historia imeandika na itabaki kukumbuka jina la Kipchoge!