Huyu Diamond hashikiki Afrika

Nyota wa Bongo Flava, Diamond Platnumz ameandika rekodi nyingine kwa kufanya shoo ya kitofauti zaidi kwenye onyesho la Africa Day Benefit Concert at Home lilioandaliwa kwa ajili ya kuchangia familia zilizoathiriwa na janga la Covid 19.
Onyesho hilo lililofanyika jana siku liliandaliwa na ViacomCBS Networks Africa, wamiliki wa chanel ya MTV Africa kushirikiana na mtandao wa Youtube pamoja na mwigizaji Idriss Elba, ambaye pia alikuwa ni mshehereshaji wa tukio hilo.
Onyesho hilo lililokutanisha zaidi ya wasanii 35 kutoka nchi 25 za Afrika walitumbuiza kutoka majumbani na kurushwa Youtube, Tanzania ikiwakilishwa na Diamond na Nandy a.k.a The African Princess.
Pia, wasanii wengine akiwemo Davido, Burna Boy na Sauti Sol walitumbuiza wakiwa studio. Lakini, Diamond alifanya tofauti kwa kutia sukari ya ubunifu.
Show yake kwanza ilianza akiwa kitandani amelala asubuhi, kisha mnenguaji wake wa kike akamletea kifungua kinywa, na baada ya hapo akatupa shuka, akainuka na kuanza kuimba wimbo wake wa "Jeje" huku yeye na mnenguaje wake wakicheza na kuuzungumka mjengo wake kuanzia chumbani, chumba cha kubadilishia nguo, chumba cha TV na kwenda kumaliza nje.
Show hiyo pia ilikuwa na ‘special appearance’ za watu maarufu kama vile Ludacris, Fat Joe, French Montana, Sean Paul, Trevor Noah, Yvonne Chaka Chaka, lakini pia ilifunguliwa kwa hotuba ya kuhimiza ushirikiano wa Afrika kutoka kwa Rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa.
“Tatizo hili limemkumba kila mtu, lakini nchi maskini zimeumia zaidi hata hivyo gharama za kurekebesha madhara hayo ni kubwa, kwa hiyo kupitia tamasha hili itakuwa ni kama mwanga na dira nzuri ya kuonyesha ushirikinao wetu sisi kama wa Afrika, kwa ajili ya Afrika.” ameeleza Rais Ramaphosa.