Huyu Bilo kwa mkwara tu

Muktasari:

Kocha huyo mwenye makeke mengi uwanjani amesema kikosi hicho kinakuja kivingine msimu ujao kwa kutoa dozi kwa kila watakayekutana naye.

Kocha wa Alliance FC, Athuman Bilal (Bilo) ameanza kuchonga sasa baada ya kuwapiga mkwara wapinzani wake kwenye Ligi Kuu Bara kuwa wajipange kutokana na usajili bora alioufanya mwaka huu.

Bilo alianza kuinoa Alliance FC miezi miwili iliyopita akichukua mikoba ya Malale Hamsini aliyetimuliwa, lakini sasa tayari ameanza kuwatia joto wapinzani wake.

Kocha huyo mwenye makeke mengi uwanjani amesema kikosi hicho kinakuja kivingine msimu ujao kwa kutoa dozi kwa kila watakayekutana naye.

Alisema msimu uliopita timu hiyo haikufanya vizuri, lakini msimu ujao chini yake kikosi hicho kitakuwa moto wa kuotea mbali.

“Tuna mechi kadhaa za kirafiki ukiwemo mchezo wa leo (jana) dhidi ya Rhino Rangers inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza, pia tutacheza na Singida United na tutatafuta mechi nyingine kabla ya ligi kuanza,” alisema Bilo.

Alisema amefanya usajili wa uhakika na tayari wachezaji wote wapya na wale wa zamani wameshazoeana, hivyo wanachosubiri ni kufanya maajabu kwenye ligi.