Hii ndo Mtibwa Sugar bwana, KCCA watatoka tu!

Muktasari:

Mtibwa Sugar imepita hatua ya awali kwa kuwatoa Northen Dynamo ya Shelisheli kwa ushindi wa mabao 5-0. Ilishinda nyumbani kwa mabao 4-0 na ugenini 1-0.

Dar es Salaam. Kocha Mkuu wa Mtibwa Sugar, Zubeiry Katwila amesema, anakwenda Uganda kwa ajili ya kutafuta ushindi na si vingine kwa sababu inawezekana.

Katwila ambaye kikosi chake kimefuzu kucheza mechi za raundi ya kwanza ya mashindano ya Kombe la Shirikisho Afrika na watakutana na KCCA mchezo ambao unatarajiwa kupigwa  Desemba 15, ugenini na marudiano ni kati ya Desemba 23-24.

Amesema, wana muda wa kutosha kwani wiki moja inatosha kufanya maandalizi mazuri wakaibuka na ushindi kama walivyokusudia.

"Tunakwenda kucheza na KCCA kama ambavyo kila mmoja anafahamu kuwa hiyo timu si ya kubeza kutokana na uwezo wao, lakini kitu kikubwa ni kujipanga tu,"alisema Katwila aliyeichezea timu hiyo ya Mtibwa kwa zaidi ya miaka 10.

Amesema, ugumu huo unaongezwa kutokana na namna timu hizo zinavyojuana na ufanano wa staili za kucheza mpira kwa sababu zote zinatoka ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.