He! Torreira naye kashtua mapema tu Emirates

Muktasari:

  • Torreira alicheza kwa dakika 45 na kutolewa na baadaye alionekana akiwa amefungwa barafu kwenye mguu wa kushoto akiwa kwenye benchi katika mechi ambayo Uruguay iliibuka na ushindi wa mabao 4-1 dhidi ya Mexico.

ARSENAL imekumbwa na hofu kubwa kuhusu supastaa wake mpya kiungo, Lucas Torreira juu ya afya ya mchezaji huyo kama ipo fiti kufuatiwa kutolewa uwanjani mapema sana alipokuwa akiitumikia Uruguay.

Torreira alicheza kwa dakika 45 na kutolewa na baadaye alionekana akiwa amefungwa barafu kwenye mguu wa kushoto akiwa kwenye benchi katika mechi ambayo Uruguay iliibuka na ushindi wa mabao 4-1 dhidi ya Mexico.

Kiungo huyo ametua Emirates kwa ada ya Pauni 22 milioni kitokea Sampdoria kwenye dirisha lililopita, hivyo kama atakuwa ameumia sana litakuwa pigo kubwa kwa Kocha Unai Emery, ambaye alikuwa akimpa dakika chache staa wake ili awe fiti kwa asilimia 100 baada ya kuchelewa kujiunga na wenzake akitokea kwenye fainali za Kombe la Dunia 2018.

Ameanzia kwenye benchi katika mechi zote nne ilizocheza Arsenal kwenye Ligi Kuu England msimu huu, huku mpango ukiwa kuanza kumtumia tangu mwanzo katika mechi zijazo.

Torreira alionekana kushirikiana vyema na Alexandre Lacazette na kupatikana kwa bao la ushindi katika mechi ambayo Arsenal iliichapa Cardiff City 3-2 ugenini.