Hazard anasema Ballon d'Or apewa Modric tu

Muktasari:

Eden Hazard ni mmoja wa wachezaji 30 waliochaguliwa kuwania tuzo ya Ballon d'Or 2018, lakini anasema ni kwamba kiungo wa Los Blancos, Luka Modric ndiye atakayekuwa mshindi

SUPASTAA, Eden Hazard ametajwa kwenye orodha ya mastaa 30 wanaofukuzia tuzo ya Ballon d'Or kwa mwaka huu.
Lakini staa huyo wa Chelsea hataki kujipigia debe mwenyewe na kumtaja mchezaji ambaye anaamini akiibuka mshindi hatakuwa kwenye mshangao. Hazard alisema anaamini kiungo wa Real Madrid, Luka Modric ndiye mshindi wa Ballon d'Or ya mwaka huu.
Staa huyo wa Kibelgiji amekuwa kwenye kiwango bora kabisa huko Chelsea akicheza kwa kiwango bora pia katika kikosi cha Timu ya Taifa ya Ubelgiji, ambayo ilifika nusu fainali ya Kombe la Dunia 2018.
Lakini Hazard anaamini mshindi ni Modric, akisema: "Luka Modric atashinda Ballon d'Or.
"Sijifikirii mwenyewe, kwa sababu siwezi kushinda. Modric anastahili. Kuna wachezaji watatu au wanne wenye nafasi kubwa, lakini Modric ataibuka mshindi. Hiyo itakuwa tuzo yake bora kutokana na mafanikio makubwa ya msimu huu.
"Kama ukiniambia nimekuwa mchezaji bora kwa miezi mitatu iliyopita, nitakubaliana na hilo bila ya shaka. Si kama napenda kusema mimi ni bora, lakini kuna Neymar, Mbappe na bila shaka kuna Messi na Ronaldo."
Tuzo hiyo imeripotiwa itatolewa Desemba mwaka huu na kwa sasa kinachofanyika ni mchakato wa wachezaji walioteuliwa kupigwa kura.