Haya Ronaldo anamtaka Mourinho huko Juve

Muktasari:

Kinachoelezwa ni kwamba mfumo aliokuwa ameutengeneza Mourinho ndio uliokuja kuendelezwa na Carlo Ancelotti na baadaye Zinedine Zidane.

TURIN, ITALIA.SI unajua Juventus kwa sasa haina kocha baada ya kumpiga kibuti Max Allegri? Basi makocha kibao wanahusishwa na kibarua cha kwenda kuwanoa mabingwa hao wa Italia, lakini supastaa wao, Cristiano Ronaldo anamtaka Jose Mourinho.

Ripoti zinadai Ronaldo anamtaka Mourinho kwa sababu anafahamu wazi Mreno mwenzake huyo ni kocha wa ushindi.

Ronaldo na Mourinho waliwahi kuwa pamoja huko Real Madrid na kupata mafanikio tena mbele ya Barcelona iliyokuwa moto chini ya Pep Guardiola.

Ronaldo anautazama msimu wa 2011-12 kuwa wenye mafanikio makubwa kwake kwa sababu akiwa kwenye kikosi cha Real Madrid waliweza kuipiku Barcelona ile iliyokuwa moto chini ya Guardiola. Kipindi hicho, Mourinho alitengeneza kikosi kilichoendana na alivyokuwa akitaka Ronaldo na ndiyo maana anamtaka aje huko Juventus wakafanye mambo tena.

Kinachoelezwa ni kwamba mfumo aliokuwa ameutengeneza Mourinho ndio uliokuja kuendelezwa na Carlo Ancelotti na baadaye Zinedine Zidane.

Mourinho aliifanya Madrid kujengwa kwa kupitia Ronaldo kitu ambacho kiliendelezwa na makocha waliofuatia huku ikielezwa kwamba sababu moja kubwa iliyomfanya Zidane ang’atuke kwenye timu hiyo mwaka jana aligundua kwamba mabosi wa Los Blancos walikuwa hawanna uwezo tena wa kumzuia Ronaldo asiondoke.