Hapo Uwanja wa Bernabeu TV hadi chooni unaambiwa!

Muktasari:

Inaelezwa kwamba miongoni mwa sababu za kuchelewa kufunguliwa Uwanja wa White Hart Lane, sababu ni kuendelea kwa mipango ya kuweka mfumo wa runinga hizo kwenye vyoo uwanjani hapo

Madrid, Hispania. Umewahi kuchanganyikiwa pindi unapotoka tu kukojoa wakati  mechi ikiendelea na ukakosa kushuhudia bao lililofungwa ndani ya nusu dakika katika kipindi cha pili?

Mbaya zaidi sio tu kwamba umekosa nafasi hiyo kushuhudia bao la mapema, pia unakuta kwamba  mtu aliyekaa kiti chako cha jirani anazungumzia  kuwa hilo ndio bao kali la msimu. Ukitafakari unagudundua kuwa umekosa kushuhudia matukio hayo muhimu kwa sababu tu, ulikuwa chooni kukojoa.

Lakini hayo yote yanaelekea kuwa na kikomo kwa  mashabiki wa klabu ya Real Madrid ambapo, kwenye uwanja wao wa Bernabeu zimeweka runinga kwenye vyoo ili kuhakikisha watu hawapitwi na kila tukio linaloendelea uwanjani.

Video tayari zimeachiwa zikionyesha jinsi ambavyo runinga hizo zinavyofanya kazi kwenye vyoo vya uwanja wa  Bernabeu.

Real Madrid sio kwamba wao ndio waanzilishi wa huduma hiyo kwa klabu za La Liga kwani hata Legunes wameweka mfumo kama huo vyooni kwenye dimba lao la Municipal de Butarque.

Hiyo ni hatua kubwa muhimu kwa klabu ya Real Madrid ambao wametumia takribani Paundi 500 kufanya ukarabati huo kwenye dimba la Bernabeu ambapo pia inahusisha ujenzi wa maghorofa mapya.

Klabu hiyo imehitimisha hatari ya kukosa matukio uwanjani, ambapo mfumo huo umeonekana kupendwa na kuwavutia watu wengi.

Iwapo itatokea shabiki alikwenda kukojoa na bao likawa limefungwa, basi runinga hiyo itamuwezesha shabiki kutokuwa na haraka kutoka chooni. Hivyo ataweza kuona  marudio wakati bao likifungwa wakati akiendelea kupata huduma yake chooni.

Huduma hiyo ambayo tayari inapatikana kwenye klabu ya Leganes, lakini inaonekana imetanuka  zaidi na hivi karibuni mashabiki wa Tottenham watakuwa miongoni mwa watu watakaofaidi teknolojia hiyo mpya.