Hadithi ya Salah, jibu kitendawili cha Samatta

JANUARI 23, 2014, Chelsea ilitangaza dili lao la kumnasa, Mohamed Salah limekubaliwa na Basel aliyokuwa akiichezea huko nchini Uswiss huku ikiripotiwa kuwa imewagharimu Pauni 11 milioni ambazo ni zaidi ya Bilioni 32 kwa fedha za Kitanzania.

Siku tatu baadaye ilitangazwa rasmi kuwa Chelsea imemsajili mchezaji huyo ambaye aliingia kwenye vitabu vya kumbukumbu vya taifa lake katika upande wa soka kwa kuwa mchezaji wa kwanza raia wa Misri kusajiliwa na mtajiri hao wa London.

Februari 8 ndani ya mwaka huo, Salah aliichezea Chelsea mchezo wake wa kwanza wa Ligi Kuu England licha ya kwamba hakuanza kikosi cha kwanza lakini alikuwa sehemu ya mchezo ambao waliibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Newcastle United.

Akiwa na Chelsea katika msimu wake huo wa kwanza, alifunga bao lake la kwanza, Machi 22 ilikuwa katika ‘London Derby’ dhidi ya Arsenal, aliingia kuchukua nafasi ya Oscar. Chelsea iliibuka na ushindi wa mabao 6-0 kwenye mchezo huo ambao ulichezwa Stamford Bridge.

Salah hakuonekana kuwa na maajabu yoyote chini ya Jose Mourinho na mwisho wa siku akatolewa kwa mkopo kwenda Italia msimu uliofuata ambako alienda kuichezea klabu ya Fiorentina. Aliichezea klabu hiyo kwa mwaka mmoja tu na kufunga mabao sita kwenye michezo 16.

Bado Mourinho hakuona kuwa ni mchezaji ambaye anaweza kuongeza kitu kwenye kikosi chake, safari ya kucheza kwa mkopo kwa Salah iliendelea na safari hiyo akapelekwa AS Roma ambako baada ya kuvutiwa naye wakaamua kumsajili moja kwa moja.

Salah alifanya makubwa huko Italia na kuanza kuimbwa na vyombo vya habari nchini humo, ni wazi pengine Mourinho alikuwa akijilaumu juu ya uamuzi aliyochukua wa kumpiga bei.

Mara akaanza kuhusishwa na klabu mbalimbali kubwa barani Ulaya ikiwemo FC Barcelona lakini katika vita hiyo, walishinda Liverpool na Juni 22, 2017 akatangazwa kuwa mchezaji rasmi wa klabu hiyo.

Tangu hapo hadi leo, nyota huyo anatajwa kuwa mmoja wa wachezaji bora na hatari kwenye kikosi cha Liverpool, ameiwezesha kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu England msimu uliopita baada ya zaidi ya miaka 30 ya ukame wa kombe hilo alikuwa na mchango mkubwa walipotwaa ubingwa Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu wa 2018/19.

Licha ya umri wa kutua England unatofautiana na nahodha wa Taifa Stars, Mbwana Samatta lakini hadithi ya nyota huyo wa timu ya taifa la Misri inaweza kuwa jibu la kitendawili chake.

Alisajiliwa kama mbadala wa Wesley Moraes ambaye kwa wakati huo alikuwa akisumbuliwa na majeraha, Samatta alijikuta akifunga bao moja tu kwenye ligi hiyo, ni wazi hakuonekana kuwa mshambuliaji hatari wa daraja ambalo walikuwa wakilihitaji.

Ndio maana mara baada ya msimu kumalizika wakaingia sokoni na kuleta mashine nyingine akiwemo, Ollie Watkins taratibu akaanza kusota benchi, nahodha huyo wa Taifa Stars na mwishowe ikaelezwa kuwa ni mmoja wa wachezaji ambao wameonyeshewa mlango wa kutokea.

Kugomewa kwa West Brom ambao ni wapinzani wa Aston Villa kumchukua kwa mkopo, Samatta hakuwa na chaguo lingine zaidi ya kukubali ofa ya kujiunga na Fenerbahce ya Uturuki.

Licha ya kwamba awali ilikuwa ikielezwa kuwa atajiunga kwa mkopo wa msimu mzima mambo yakawa tofauti Waturuki wakaamua kumsajili moja kwa moja mshambuliaji huyo wa Kitanzania.

Kutau kwa Samatta Fenerbahce sio ndio mwisho wa safari yake kwa umri wa 27 aliyonayo bado ananafasi ya kurejea EPL na kuonyesha makali yake kama ilivyokuwa kwa Salah ambaye kwa sasa hashikiki.

Mbali na Salah ambaye umri wake wakati akiondoka ulikuwa ukiruhusu ipo mifano ya wachezaji ambao waliondoka na umri wa Samatta na kurejea kwa namna nyingine kwenye ligi hiyo kama vile mshambuliaji wa Nigeria, Odion Ighalo.

Ighalo alikuwa akiichezea Watford lakini baadaye akiwa na umri kama wa Samatta akaamua kwenda zake kupiga pesa China kwa kuzichezea Changchun Yatai na Shanghai Greenland Shenhua lakini kwa sasa yupo wapi? Amerejea zake England tena yupo klabu (Man United) ya daraja la juu zaidi ya ile ambayo alikuwa akiichezea awali.