H Baba aipa mchongo Gwambina FC

Muktasari:

Gwambina FC ya Misungwi mkoani Mwanza, imekuwa timu ya kwanza ya Ligi Daraja la Kwanza msimu huu kupanda Ligi Kuu baada ya kuongoza kundi B la Ligi Daraja la Kwanza

MSANII wa Muziki wa kizazi kipya, Hamisi Ramadhani ‘H Baba’ amesema kama Gwambina FC watajipanga vyema msimu ujao kwa kufanya maandalizi ya nguvu basi itakuwa timu tishio katika Ligi Kuu.

Gwambina FC ya Misungwi mkoani Mwanza, imekuwa timu ya kwanza ya Ligi Daraja la Kwanza msimu huu kupanda Ligi Kuu baada ya kuongoza kundi B la ligi hiyo.

Akizungumza na Mwanaspoti Online, H Baba ambaye aliwahi kucheza soka hapo nyuma hasa katika timu ya Toto Africans, alisema ameona timu hiyo ina mipango mizuri na kama wakijipanga kwa kufanya usajili wa mzuri basi msimu ujao itaweza kuzitesa Simba na Yanga ambazo zinatamba kwa sasa Ligi Kuu.

“Ninawashauri wafanye usajili wa mzuri wasikurupuke unajua Ligi Kuu ina ushindani sana hivyo wanatakiwa kujiandaa sana kwangu naona wataleta ushindani sana msimu ujao kwani ni timu inaonekana imejipanga vizuri.

Kikubwa sisi kama wadau wa soka Mwanza tunatakiwa kuipa ushirikiano hii timu kwani naiona inaweza kuupa sifa kubwa mkoa wetu kwenye Ligi Kuu msimu ujao kama wanavyofanya Namungo na Polisi Tanzania kwa sasa,” alisema H Baba.

Alishauri timu hiyo kuongeza nguvu kwenye safu ya ushambuliaji,kiungo na ulinzi kwa kuwasajili wachezaji wazoefu watakaoisadia kupata mafanikio.

“Unajua Ligi Kuu ni ngumu sana hivyo kinachotakiwa ni kuwa na kikosi kipana chenye wachezaji wazuri mimi nawafatilia sana Namungo na Polisi Tanzania unajua walisajili wachezaji wazoefu ambao ndio wanaofanya timu hizo ziwe bora msimu huu,” alisema.