Gwambina yafunga na 25 akiwamo Kipa Mzambia

Muktasari:

Gwambina imefunga zoezi la usajili kwa wachezaji 25 akiwamo Kipa mmoja kutoka nchini Zambia kwa ajili ya kuitumikia timu hiyo msimu ujao.

KLABU ya Gwambina FC imefunga usajili wake na sura mpya 10 ikiwamo kipa Stali Nyambe raia wa Zambia kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Bara inayotarajia kuanza Septemba 6 mwaka huu.

Timu hiyo ya jijini hapa inatarajia kushirikia Ligi Kuu ikiwa ni msimu wake wa kwanza, ambapo katika kikosi kizima asilimia kubwa ni wachezaji walioipandisha daraja.

Kupitia akaunti ya Klabu hiyo, imeonyesha jumla ya wachezaji 25, ambapo 11 ni wapya kutoka timu tofauti na 14 wakiwa ni wale walioiwezesha kushiriki ligi hiyo mapema mwezi ujao.

Kikosi hicho kinajumuisha Makipa; Mohamed Makaka (Ruvu Shooting), Isihak Ibrahim na Mohamed Hussein (Gwambina) pamoja na Nyambe kutoka Buildcon ya nchini Zambia.

Mabeki ni Revocatus Mgunga, Salum Kipaga, Hamad Nassor, Anthony Matogoro(Gwambina), Aron Lurambo (KMC), Lameck Daniel, (Biashara United), Baraka Mtui (Ruvu Shooting) na Novatus Lufunga wa Lipuli.

Viungo ni Yusuph Kagoma, Yusuph Lwenge, Salim Juma, Rajabu Athuman na Jacob Masawe (Gwambina), Said Mkangu aliyetoka Sahare All Stars iliyoshuka Ligi Daraja la Pili (SDL).

Washambuliaji ni Meshack Abraham, Jimmyson Steven na Kapama Kibaden (Gwambina), Moric Mahela na Miraj Saleh (Stand United), Japhet Makalai (Kagera Sugar) na Paul Nonga kutoka Lipuli.

Katibu Mkuu wa Klabu hiyo, Daniel Kirai amesema hadi sasa tayari wachezaji wote wamewasili na wanaendelea na mazoezi katika uwanja wa Shule ya Msingi Mitindo wilayani Misungwi, wakati uwanja wao ukiendelea kufanyiwa marekebisho.