Gwambina FC kunoa makali kwa Mwadui leo

Muktasari:

Gwambina FC msimu uliopita ilikuwa ikitambulika kwa jina la Arusha United ni moja ya timu inayopewa nafasi ya kufanya vizuri msimu huu

Dar es Salaam. Vijana wa Kocha, Novatus Fulgence wanatarajia kushukua uwanjani leo Jumatano kukipiga na Mwadui FC kwenye Uwanja wao wa nyumbani.

Katibu Mkuu wa timu hiyo, Daniel Kirai alisema wanatumia michezo hiyo kukiandaa kikamilifu kikosi chao ili kukimbizana na ratiba ya kocha pamoja na maandalizi ya Ligi Daraja la Kwanza (FDL) inayotarajia kuanza mwezi ujao.

"Gwambina ni moja ya timu iliyoingia kambini mapema kuliko timu yoyote ili kuhakikisha vijana wetu wanakuwa na muunganiko wa pamoja na kuelewana kwa haraka, kwani itamsaidia kocha kujua wachezaji watakaounda kikosi chake cha kwanza kutokana na usajili uliofanywa," alisema Kirai.

Aliongeza leo la uongozi ni kuhakikisha timu hiyo inafanya vizuri na kupanda Ligi Kuu msimu ujao ili kuongeza hamasa kwa wakazi wa mkoa huo na vijana kupata ajira kupitia timu hiyo.

Gwambina FC ambayo msimu uliopita ilikuwa ikitambulika kwa jina la Arusha United ni moja ya timu inayopewa nafasi ya kufanya vizuri msimu huu, kutokana na uwekezaji unaofanywa hasa kwa kumiliki uwanjwa wao binafsi.