Guardiola afuatilia nyendo za Kocha Man United

Muktasari:

Solskjaer mwezi uliopita alichaguliwa kuwa kocha wa muda huko Old Trafford baada ya wababe hao kumfuta kazi Jose Mourinho na tangu mabadiliko hayo yalipofanyika, Man United imekuwa tofauti na kucheza soka matata kabisa.

MANCHESTER, ENGLAND. PEP Guardiola amefichua kwamba anafuatilia kwa karibu sana kile anachokifanya kocha Ole Gunnar Solskjaer huko kwenye kikosi cha Manchester United.

Solskjaer mwezi uliopita alichaguliwa kuwa kocha wa muda huko Old Trafford baada ya wababe hao kumfuta kazi Jose Mourinho na tangu mabadiliko hayo yalipofanyika, Man United imekuwa tofauti na kucheza soka matata kabisa.

Guardiola, ambaye ni kocha wa Manchester City, mahasimu wakubwa wa wababe hao wa Old Trafford, amesema Solskjaer ana kila sababu ya kuwana furaha kutokana na kuwa na mwanzo mzuri kabisa katika ajira yake hiyo ya ukocha kwenye kikosi hicho.

Kocha Solskjaer ameshinda mechi zote tano za mwanzo alizoisimamia timu hiyo kwenye mechi za Ligi Kuu England na Kombe la FA, Man United imeshinda mechi nne za ligi na moja ya FA.

Na Guardiola alisema: “Bado ni kocha kina. Solskjaer amekuwa akifanya vizuri sana.

“Hilo linaonekana kwenye mambo yote, matokeo na timu inavyocheza. Mwanzo wake ni mzuri kuliko ulivyokuwa wangu wakati naanza ukocha. Mimi nilipoteza mechi yangu ya kwanza na kupata sare nyingine, lakini Solskjaer yeye ameshinda zote tano za mwanzo.”