Griezmann azuia dili la Neymar

Muktasari:

Mfaransa huyo amesema: “Tunapaswa kulikamilisha kwanza dili hilo kwa sababu ni uhamisho wenye ugumu sana, lakini yeye Neymar ni mchezaji mkubwa.

BARCELONA, HISPANIA.NGOMA ngumu. Ndicho unachoweza kusema kuhusu dili linalotarajiwa la Neymar kurejea Barcelona akitokea PSG.

Barca tayari wameshatumia pesa nyingi zaidi ya Euro 225 milioni kunasa saini za nyota kadhaa akiwamo Antoine Griezmann (€120 milioni) na Frankie de Jong (€75 milioni) katika kipindi hiki cha uhamisho.

Griezmann ambaye alimwaga magozi baada ya kuona usajili wake umekamilika wa kutua Barca akitokea Atletico Madrid, ametia neno kuhusu dili la Neymar, 27, kutua Barca.

Mfaransa huyo amesema: “Tunapaswa kulikamilisha kwanza dili hilo kwa sababu ni uhamisho wenye ugumu sana, lakini yeye Neymar ni mchezaji mkubwa.

“Alipata majeraha mara kadhaa lakini yuko katika kiwango cha juu kabisa.

“Pia tunaye (Ousmane) Dembele, (Philippe) Coutinho na Malcom, ambao pia ni wachezaji muhimu kwetu, hivyo acha tuone itakuwaje huku tukiombea tupate mafanikio tukiwa nao.”

Mastaa wawili ambao Griezmann hakuwataja katika orodha hiyo ni Lionel Messi na Luis Suarez.

Mshindi mara wa tuzo ya Ballon d’Or Messi na straika wa Uruguay Suarez wanatarajiwa kuendelea kuzitesa nyavu za wapinzani msimu huu bila ya kujali kama nyota wapya watasajiliwa.

Griezmann tayari ameeleza furaha yake ya kujiunga na wakali ambao ni kati ya vipaji bora zaidi vya soka duniani.

“Natumai nitakuwa na mchango muhimu, nataka kuwa mchezaji muhimu kwenye timu na kusaidia kutokea nafasi yoyote nitakayochezeshwa uwanjani,” aliongeza Griezmann.