Gor Mahia walivyopunguza visirani vya Waarab Kasarani

Muktasari:

  • Gor watasafiri nchini Algeria kumenyana na jamaa hawa mapema Jumapili ijayo. Petro Atletico ya Angola ilitoka sare ya 1-1 na Zamalek ya Misri kwenye mechi nyingine ya kundi hili.

Nairobi. Mabao ya Francis Kahata na Jacques Tuyisenge yalipunguza visirani vya Husseij Dey ya Algeria walipolazwa 2-0 na Gor Mahia uwanjani Kasarani juzi Jumapili kwenye dimba la kombe la mashirikisho.

Kahata alifunga bao la ufunguzi dakika ya 86 akimalizia krosi ya Shaffik Batambuze kabla ya Tuyisenge kuongeza mpigo wa ngoma za halaiki ya mashabiki wa Gor na bao la pili dakika ya 88.

Gor sasa imerejesha uongozi wake kwenye jedwali hilo la kundi D na pointi sita, mbili nyuma ya Waarab hao ambao wamepoteza mechi ya kwanza kabisa katika michuano hii.

Kisirani ya wageni ilianza kipindi cha kwanza wakati nahodha wao Ahmed Gasmi aligongana na winga wa Gor Samuel Onyango akikimbishwa hospitalini Aga Khan. Kiungo wao Hocime Orfi pia akatolewa dakika ya 37 na jeraha lingine.

Baadaye Chems Harrag akaonyeshwa kadi nyekundu dakika ya 87 kwa kumtusi mwamuzi.

Katika ya bao la pili benchi la Hussein Dei walivuragana na la Gor kuhusu vichupa vilivyorushwa uwanjani na wafuasi wa Gor kabla ya mechi komesaya kuingilia kati na kuruhusu mechi kumalizika.

“Tulifahamu kwamba ni timu nzuri ambayo inajivunia ufadhili mzuri,” anasema kocha wa Gor Hassan Oktay.

“Lakini tuliwafanyia utafiti vilivyo na kufahamu upungufu wao na hapo ndio tulishindia mechi hiyo. Tukisafiri ugenini, tumewaona zaidi tutajituma kupata angalau sare.”

Gor watasafiri nchini Algeria kumenyana na jamaa hawa mapema Jumapili ijayo. Petro Atletico ya Angola ilitoka sare ya 1-1 na Zamalek ya Misri kwenye mechi nyingine ya kundi hili.

Sasa Petro na Hussein Dey wana pointi nne huku Zamalek ikiwa nafasi ya mwisho na alama mbili tu.

Kabla ya kusafiri nchini Algeria, Gor itachuana na Tusker kwenye mechi ya ligi hapo kesho ugani Kasarani.