Giniki karudi, mjipange tu sasa!

Muktasari:

Giniki ambaye ni mpwa wa wanariadha wakongwe, Gidamis na Alfredo Shahanga ambao ndio wanamsimamia mara nyingi pamoja na Kocha wa Timu ya JWTZ, Anthony Muingereza, mara ya mwisho kushiriki mashindano yalikuwa yale ya Majeshi ya Dunia yaliyofanyika mwezi uliopita China.

MWANARIADHA wa mbio fupi, Emmanuel Giniki amesema ameanza mazoezi ya taratibu baada ya kuwa majeraha kwa muda wa wiki kadhaa na sasa anauweka mwili sawa kutokana na kuwa na tatizo la misuli akiwa mazoezini.

Giniki alisema majeraha aliyoyapata yamesababisha kushindwa kutafuta mbio mwishoni mwa mwaka huu kama ilivyokuwa kwa miaka ya hivi karibuni alivyokuwa akifanya kwa kushiriki mashindano tofauti.

“Kwa muda mrefu nilikuwa nimepumzika na sasa ndio nimeanza mazoezi taratibu ili kuuweka mwili sawa kabla ya kuanza kutafuta mashindano mbalimbali yatakayozidi kuniweka fiti kimwili na kwenda kushindana mbio za nje,” alisem Giniki.

Aliongeza mapema mwaka ujao ataanza harakati za kusaka viwango vya kwenda kushiriki Mashindano ya Olimpiki yatakayofanyika Tokyo, Japan na hilo atahakikisha anajifua zaidi ili kuwa kwenye msafara wa wa kwenda Japan.

Giniki ambaye ni mpwa wa wanariadha wakongwe, Gidamis na Alfredo Shahanga ambao ndio wanamsimamia mara nyingi pamoja na Kocha wa Timu ya JWTZ, Anthony Muingereza, mara ya mwisho kushiriki mashindano yalikuwa yale ya Majeshi ya Dunia yaliyofanyika mwezi uliopita China.

Mwingereza alisema kwa mwanariadha kupatwa na matatizo ya misuli ni jambo la kawaidia na Giniki anaendelea vizuri na mazoezi na muda sio mrefu atarudi kwenye kasi yake na kuingia kwenye mashindano kama kawaida.

“Tunaendelea kuwaweka wanariadha sawa kwa sababu mbele yetu kuna mashindano ya Jaica yatakayofanyika Dar es Salaam kwa siku mbili kuanzia Desemba 7 na 8, hivyo wanapokuwa fiti inasaidia kuwa na wanariadha wenye ushidani wakati wote,” alisema Muingereza .