Giggs ashikiliwa na polisi

MANCHESTER, ENGLAND. MCHEZAJI wa zamani wa Manchester United, Riyan Giggs amekanusha ripoti za kufanya unyanyasaji wa kijinsia kwa mchumba wake Kate Greville kwenye jumba lake lenye thamani ya   Pauni 1.7 milioni huko Jijini Manchester baada ya kukamatwa na polisi.

Ripoti zinadai kwamba polisi walipata taarifa hizo majira ya 4:00 asubuhi juu ya kuwepo kwa vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia katika jumba hilo na wakafunga safari, kwenda kumkamata Giggs ambaye alikana tuhuma hizo baada ya kufanyiwa mahojiano.

Wakala wa mwanasoka huyo ambaye kwa sasa anakinoa kikosi cha timu ya Taifa ya Wales alisema  Giggs amekanusha tuhuma zote za unyanyasaji wa kijinsia kwa mpenzi wake na anaendelea kushirikiana na polisi ili kuwasaidia kufanikisha uchunguzi wao.

Kufuatia taarifa hizo chama cha soka cha  Wales 'FAW' kilisitisha mkutano wake na waandishi wa habari uliokuwa na ajenda ya kutangaza kikosi ambacho kitakwenda kujichimbia kambini kwa ajili ya maandalizi ya michezo dhidi ya USA, Finland na Jamhuri ya Ireland.

Wawili hao wamekuwa kwenye migogoro ya hapa na pale tokea mwaka 2017. Ikiwa walikutana mwaka 2013 ambapo mwanamama huyo aliajiriwa kwenye Hotel ambayo Giggs ni mmiliki msaidizi.

Polisi wa Jiji la Manchester walithibitisha kwamba kweli walimkamata Giggs mwenye umri wa miaka 46, lakini aliachiwa kwa dhamana baada ya kufanyiwa mahojiano ya kina sambamba na kufunguliwa kwa jalada la uchunguzi kuhusiana na tukio hilo.

Giggs na Greville walionekana hadharani kwa mara ya kwanza mwaka 2018, wakiwa nchini Italia ambapo walikwenda kuponda raha ikiwa ni muda mchache baada ya Giggs kumpa talaka aliyekuwa mke wake   Stacey mwezi Desemba mwaka 2017.