Fifa kumpiga msasa mwamuzi Mtanzania

Dar es Salaam. Mwamuzi msaidizi Soud Lila, ataiwakilisha Tanzania katika kozi maalum ya kimataifa ya waamuzi wa soka itakayofanyika Uganda kuanzia Septemba 14 hadi Septemba 18.

Kozi hiyo inashirikisha jumla ya waamuzi wachanga 34 kutoka nchi mbalimbali barani Afrika ambao wana beji ya Shirikisho la Soka Duniani (FIFA).

Kwa mujibu wa taarifa kutoka Shirikisho la Soka Afrika (CAF) wanaosimamia na kuendesha kozi hiyo, idadi ya jumla ya waamuzi hao itajumuisha marefa wa kati, washika vibendera na waamuzi wa kike.

Idadi ya marefa wa kati watakaoshiriki kozi hiyo ni 15 ambayo itakuwa sawa na waamuzi wa pembeni huku waamuzi wa kike wakiwa ni wanne.