Fei Toto afunguka mzimu wa kadi unavyomuandama uwanjani

Muktasari:

  • Fei Toto ambaye msimu huu ni kwanza kwake ndani ya Yanga, anasema kuna wakati ambao anatambua kosa linalomfanya adhibiwe na mwamuzi, lakini wakati mwingine zinakuwa zinaacha maswali ndani yake.

KIUNGO wa Yanga, Fei Toto ambaye anahusishwa na kutaka kutimkia Uingereza kucheza soka la kulipwa, amefunguka sababu ya kulimwa kadi mara kwa mara kwamba inamshangaza wakati mwingine haelewi zinatokana na nini.

Fei Toto ambaye msimu huu ni kwanza kwake ndani ya Yanga, anasema kuna wakati ambao anatambua kosa linalomfanya adhibiwe na mwamuzi, lakini wakati mwingine zinakuwa zinaacha maswali ndani yake.

"Siwezi kusema ni presha ya ligi kwani naona mechi ni zakawaida hasa kwa mchezaji ambaye anatambua majukumu yake kikamilifu ndani ya uwanja.

"Makocha wanakuwa wametuelekeza ya kufanya wakati wa mechi na ndio maana tunakuwa tunafanya mazoezi ambayo yanakuwa yanaonyesha ubora na madhaifu yetu"anasema.

Fei Toto ni kati ya wachezaji ambao wanaongoza kwa kupata kadi kwa msimu huu, jambo ambalo amesema sio zuri kwani linakuwa linachafua jina lake ingawa anasisitiza kuna wakati zinatokea bila ya yeye kukusudia.

"Pia siwezi kusema uwezo wangu ndio chanzo cha mimi kukamiwa kwani mpira wa miguu kila timu inakuwa ina malengo ya kupata pointi tatu dhidi ya mwingine,"anasema.