Farid aitaka Simba

NYOTA wa Yanga SC, Farid Mussa ameonyesha hamu kubwa ya kucheza mechi ya watani wa jadi Simba SC na ameweka wazi kwamba anapenda kucheza mechi ngumu za aina hiyo, zinazomfanya aonyeshe makali na kutumia nguvu.

Amesema kama atapata nafasi ya kuwemo kwenye kikosi kitakachocheza na Simba, Novemba 7, 2020 utakaopigwa Uwanja wa Benjamini Mkapa zamani uliokuwa unaitwa Taifa, itakuwa furaha kwake kuonyesha ufundi katika mchezo unaotazamwa na wengi.

Mwanaspoti iliwahi kuzungumza na Farid kipindi cha nyuma katika makala maalumu, mchezo huo ukiwa umekaribia amegusia jambo hilo kwamba hauogopi na anautamani ili kudhihirisha madini yaliopo mguuni kwake.

"Niliwahi kucheza dhidi ya Simba na Yanga wakati huo nikiwa Azam lakini  safari nii natambua kuwa itakuwa tofauti. Siku zote nimekuwa nikipenda michezo mikubwa kwa sababu kwangu hilo ndio jukwaa la kuonyesha kipaji changu,"  amesema Farid na ameongeza kuwa,

"Natambua ni mechi ngumu inayohitaji utulivu, kujituma na ufundi zaidi, pia ina presha kubwa ya mashabiki, ninachopenda ni aina ya mpira wa ushindani unaokuwa unachezwa,"amesema.

Farid  alijiunga na Yanga akitokea CD Tenerife ya Hispania kwa kusaini mkataba wa mwaka mmoja ambao anaamini unatosha kwake kuonyesha makali yake kabla ya kwenda nje tena kupigania ndoto zake.

Alitueleza hivyo wakati ambao tulifanya naye mahojiano kwa mara ya kwanza  mara baada ya kusaini mkataba huo wa kuitumikia timu hiyo ya Wananchi yenye makao yake makuu Jangwani, Dar es Salaam.

Kabla ya Yanga kuonyesheana ubabe dhidi ya Simba watakuwa na kibarua kizito leo jioni Novemba 3, Jumanne cha kucheza dhidi ya wenyeji wao, Gwambina jambo ambalo amesema wamejipanga na wanaheshimu kila mchezo kihakikisha wanavuna pointi tatu.