FA yazipeleka timu za Arusha Ligi Kuu Bara

Muktasari:

Madini Pekee ndio yenye historia ya kufanya vyema kwenye ligi hiyo baada ya msimu ulipita kutinga hadi hatua ya robo fainali baada ya kutolewa na Simba kwa kufungwa bao 1-0

Arusha. Droo ya mzunguko wa pili wa michuano ya FA iliyofanyika Jumatano imezefanya timu nne kati ya tano za mkoani hapa kujikuta zikiangukia midomoni mwa timu zinazoshiriki Ligi Kuu Bara, huku Maafande wa Oljoro pekee wakisubiri kuvaana na timu inayoshiriki Ligi ya Mabingwa wa Mikoa.

Mkoa wa Arusha unawakilishwa na timu ya JKT Oljoro inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza (FDL), Madini SC, Pepsi FC, na Arusha FC zote za SDL huku timu ya Bodaboda ya wilayani Karatu ikiwa ipo Ligi ya Mabingwa wa Mikoa (RCL).

Pamoja na kuangukia kwenye timu za Ligi Kuu bado timu zote zitakuwa ugenini kwenye ligi hiyo Oljoro akivaana na Ambassador ya Kahama, Madini SC dhidi ya Ruvu Shooting, Pepsi na Mwadui, Arusha Fc akiifuata Standi Utd wakati Bodaboda ikivaana na Singida Utd.