Eto'o akaribishwa na Madafu Dar

Muktasari:

Kesho Alhamisi, Eto'o, Ndour na Mapunda watazindua kiwanja kipya cha soka cha wachezaji watano watano kilichojengwa kwa udhamini wa Bia ya Castle

Eto'o ni miongoni mwa nyota maarufu wa soka barani Afrika kutokana na uhodari wake wa kufumania nyavu katika klabu za Barcelona, Real Mallorca, Chelsea na Anzhi.

Mshambuliaji wa zamani wa Cameroon na Barcelona, Samuel Eto'o amekoshwa na maji ya madafu aliyokunywa saa chache baada ya kutua nchini.

Eto'o ambaye alitua nchini mchana akiwa sambamna mwanasoka wa zamani wa Senegal, Alassane Ndour, alikutana na sapraizi hiyo katika Hoteli ya Ramada ambako amefikia kwa ajili ya ziara yake nchini iliyoanza leo.

Muda mfupi baada ya kuwasili akiwa pamoja na Ndour sambamba na kipa wa zamani wa Taifa Stars, Yanga na Simba, Ivo Mapunda ambao wote ni mabalozi wa Bia ya Castle Lager, Eto'o alipewa dafu hilo na mmoja wa wahudumu wa hoteli hiyo na baada ya kunywa maji yake alionekana kufurahia huku akicheza wimbo aliokuwa akiimbiwa.