Eti Zidane hataki kazi Man United

Muktasari:

Alain Migliaccio ambaye ni wakala wa Zinedine Zidane ameibuka na kudai mteja wake wala hana mpango wa kwenda kuwa kocha wa Man United kwa sababu soka la England sio mikato yake.

MANCHESTER, ENGLAND. Kuna stori zinadai hivi, Manchester United imemwambia Zinedine Zidane avumilie kwanza kabla ya kufanya uamuzi wao wa kumfuta kazi Jose Mourinho ili akabidhiwe kazi ya kuwanoa wakali hao wa Old Trafford.
Lakini wakala wa kocha huyo wa zamani wa Real Madrid, Alain Migliaccio ameibuka na kudai mteja wake wala hana mpango wa kwenda kuwa kocha wa Man United kwa sababu soka la England sio mikato yake.
Wakala huyo alisema hakuna chochote kitakachotokea kuhusu kocha huyo kwenda Man United na hicho kinachoelezwa ni uvumi tu.
Akizungumza na JDD, Migliaccio alisema: “Manchester United? Sidhani kama atakwenda England kufundisha mpira, sio mikato yake.
"Nilizungumza naye, haonekani kabisa kuvutiwa na kibarua hicho."
Hata hivyo, wachambuzi wa mambo ya soka wanasema wakala huyo na Zidane wanaleta ujanja tu kwa sababu kimsingi hawawezi kuizungumzia kazi ambayo kwa sasa bado ina mwenyewe, hivyo kwa heshima wanalazimika kukanusha, wakati kila kitu kipo wazi, kibarua cha Old Trafford kinawavutia.
Majuzi kulikuwa na taarifa Zidane anajipa nafasi kubwa ya kwenda kuwa kocha wa Juventus na si Man United.
Hata hivyo, kama jambo hilo likitokea, basi Man United itakuwa imempata mtu wao kwani kocha mwingine anayetajwa atatua Old Trafford kama Mourinho atafutwa kazi ni Max Allegri wa Juventus.