Eti Paul Pogba ndo tatizo Man United

Muktasari:

Hata hivyo, tetesi zilizopo ni kwamba mchezaji huyo anaweza kutua katika kikosi cha Real Madrid msimu unaokuja.

MANCHESTER,England.NYOTA wa zamani wa Hull City, Liam Rosenior kaibuka na kusema tabia za Paul Pogba pale Manchester United hazikumwathiri yeye mwenyewe kama mchezaji bali pia zimeathiri wachezaji wenzake.

“Pogba si aina ya mchezaji ambaye Manchester United inamhitaji kwa sasa, timu inahitaji mtu mwenye tabia nzuri. Tabia zake mbaya zimeathiri wachezaji wenzake kisaikolojia.

“Ni kweli ana kiwango kikubwa cha kucheza mpira, lakini tabia huwa ni jambo kubwa sana katika maendeleo ya mtu yeyote.

“Ukiangalia kwa undani utafahamu timu yenye nidhamu ndio ambayo inaweza kupata mafanikio kwa urahisi sana.

“Liverpool na Manchester City zina nidhamu ya hali ya juu na hilo ndilo limefanya timu hizo zipige hatua kubwa. Hata manahodha wa timu huwa wanafanya wachezaji walio karibu yao wajione wa muhimu. Lakini ukija kwa Pogba si mfano wa kuigwa. “Tulikuwa na matarajio makubwa kutoka kwake, lakini je tuliyapata kama tulivyotaka? Hakuna kitu kama hicho.

“Pogba hakuwa kiongozi lakini mashabiki na viongozi wa Manchester United walimwamini, matokeo yake ndio hayo.”

Hata hivyo, tetesi zilizopo ni kwamba mchezaji huyo anaweza kutua katika kikosi cha Real Madrid msimu unaokuja.