Duh! Mabao 449 siyo mchezo

Muktasari:

Ukiachana na Simba, Yanga na Azam FC kufungwa idadi hiyo ya mabao mpaka sasa, Singida United ndio iliyofungwa mabao 35 mengi zaidi kuliko timu nyingine yoyote ya Ligi Kuu Tanzania Bara.

MPAKA dakika hii unavyosoma hapa mabao 449 yamefungwa kwenye Ligi Kuu Bara huku wataalamu wakisema tatizo ni mawasiliano mabovu kati ya makipa na mabeki wao.

Februari 20 ambayo ni jana Alhamisi, msimu ulioisha safu za ulinzi za ligi hiyo zilikuwa zimefikisha mabao 450, huku Ruvu Shooting ikiwa imetikiswa maraa 33 idadi kubwa ya mabao kuliko timu nyingine na ilikuwa imecheza mechi 27.

Katika mabao 450, Simba, Yanga na Azam FC zilikuwa zimefungwa mabao 33 ambapo sawa na wastani wa mabao 14.

Takwimu hizo zilionyesha Simba ilicheza mechi 16 ikafungwa mabao matano, Yanga ilikuwa imecheza michezo 24 iliruhusu mabao 16 na Azam ilicheza mechi 23 ilikuwa imetikiswa mara 12 ambapo jumla yake ilikuwa zimefungwa mabao 33.

Katika msimu huu, mpaka jana Alhamisi safu za ulinzi za VPL zilikuwa zimefikisha idadi ya mabao 449, Yanga ikiwa imeruhusu mara 18, Simba mara 11 na Azam FC mara 15.

Simba, Yanga na Azam FC zina jumla ya mabao 44 ya kufungwa, huku timu zilizobaki zikiwa zimefungwa 405,ambayo yakichanganywa kwa pamoja yanafikia idadi ya 449.

Yanga imeruhusu mabao 18 katika mechi 21 iliyocheza, Simba imetikiswa mara 11 katika mechi 23 na Azam FC imefungwa mabao 15 katika mechi 23 ilizocheza.

Ukiachana na Simba, Yanga na Azam FC kufungwa idadi hiyo ya mabao mpaka sasa, Singida United ndio iliyofungwa mabao 35 mengi zaidi kuliko timu nyingine yoyote ya Ligi Kuu Tanzania Bara.

TATIZO NINI?

Aliyekuwa kocha wa makipa wa Simba, Idd Pazi ‘Father’ alitaja udhaifu wa makipa wa ligi ya VPL k wa kushindwa kuzungumza na mabeki na kusababisha kufungwa mabao kizembe.

“Ili ligi iwe na ushindani na mvuto, lazima safu zote zifanye kazi yake kwa umakini kwa takwimu hizo inaonyesha dhahiri safu ya ulinzi ni dhaifu.

“Mfano bao alilofungwa kipa wa Yanga, Metacha Mnata dhidi ya Mbeya City, alishindwa kuzungumza na beki wake Lamine Moro ambaye alikuwa anampa mpira kwa bahati mbaya wakajifunga huo ndio uzembe uliopo kwa walinda milango wengi,”alisema.

Kipa wa Mtibwa Sugar, Said Mohamed ‘Nduda’ alikiri asilimia kubwa ya makipa ni chipukizi, hivyo ni waoga kuwakemea mabeki ama kuwapa maelekezo ya namna ya kujilinda wasifungwe.

“Binafsi huwa nawakemea mabeki wa timu yangu kuanzia mazoezini, nawaambia kabisa wasifanye ujinga ambao unaweza kutugharimu wakati wa mechi, tukizungumzia kwa ujumla sasa lazima makipa tubadilike ili tupunguze makosa ili tusipate aibu mwisho wa msimu,” alisema Nduda.

Beki wa KMC, Abdallah Mfuko alisema mbali na tatizo la makipa lakini washambuliaji wapo kwenye viwango vya juu.

“Mfano straika ya Simba ina ushindani yenyewe kwa yenyewe, ama Lipuli unadhani wakienda kucheza na wapinzani inakuaje?”