Dodoma Jiji FC yakomba wachezaji Azam, Lipuli, Alliance

Muktasari:

Dirisha la usajili limefungwa usiku wa kuamkia leo Alhamisi ambapo timu za Ligi Kuu, daraja la kwanza na pili zimeongeza na kuacha baadhi ya wachezaji.

Dodoma. Dodoma Jiji FC imefunga usajili kwa kusajili wachezaji nane wakiwemo wa kutoka Azam, Lipuli, Alliance huku ikiwatema saba katika dirisha dogo la usajili lililofungwa usiku wa kuamkia leo Alhamisi.

Dodoma Jiji fc inayoshiriki ligi daraja la kwanza imewasajili Steven Maganga (Lipuli), Ramadhani Mohamed (Azam), Ismail Makoroso (Alliance) na kipa Yusuph Abdul (African Lyon).

Wengine ni Omary Kanyoro (Geita Gold), Aziz Gilla (Sahare All Stars), Mohamed Kilua na Moka Shaban ambao walikuwa huru.

Pia, miamba hiyo imewaacha wachezaji saba walishindwa kukidhi malengo ya timu hiyo raundi ya kwanza.

Wachezaji saba waliotemwa ni Ally Ahmed "Shiboli", Khalid Juma, Jeremiah Haule, Juma Mnyasa, Kassim Kilungo, Mussa Kirungi na Mwinyi Saidi.

Katibu wa timu hiyo Fortunatus John amethibitisha usajili huo na kwamba umezingatia matakwa ya benchi la ufundi kulingana na mapungufu yaliyoonekana raundi ya kwanza.

Timu hiyo itacheza mchezo wake wa kwanza ya raundi ya pili ya ligi daraja la kwanza dhidi ya Cosmopolitan Jumamosi hii kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.