Dante katua KMC

BEKI Andrew Vicent 'Dante' amesaini mkataba wa mwaka mmoja kuitumikia KMC kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Bara.

Taarifa ambazo Mwanaspoti Online imezipata leo Jumanne Agosti 11, 2020 ni kwamba mchezaji huyo amesaini mkataba huo leo mchana katika ofisi za Halmashauri ya Kinondoni ambapo ndipo Makamu Makuu ya klabu hiyo.

Usajili wake unaenda kuongeza nguvu safu ya ulinzi ambayo alikuwa anacheza Abdallah Mfuko na Ismail Gambo ambaye mara kwa mara amezoeleka kucheza kama kiungo mkabaji.

Mtu wa karibu na mchezaji huyo aliithibitishia Mwanaspoti Online kwamba mchezaji huyo alienda kumalizana na KMC.

"Kweli ameondoka nyumbani kwenda kumalizana na KMC, walishaongea sana kwenye simu kilichobaki ni kusaini," kilisema chanzo hiko.

Alipotafutwa Dante ili kuthibitisha taarifa hizo amesema kwa kifupi "Nipo njiani kuna sehemu natoka nikitulia nitakucheki,".

Dante ni miongoni mwa wachezaji waliomaliza mikataba Yanga na kisha hawakupewa mikataba mingine ya kuendelea nao kwa msimu ujao.