Chid Benz: Wokovu siujui naokoka vipi!

Muktasari:

Chid ameliambia Mwanaspoti kuwa kwa sasa ameacha kutumia dawa za kulevya, lakini anashangaa baadhi ya watu kuendelea kumchukua kama mtu anayeendelea kutumia.

HIVI umewahi kukutana na moto wa rapa Chid Benz a.k.a Chid Benzino, ambaye anatamba na ngoma ya Dar Stand Up, ameibuka na kutangaza kuwa hajaokoka na hawezi kufanya hivyo kwa sasa.

Chid, ambaye kwa siku za karibuni amekuwa kwenye bifu la kurushiana maneno makali na Dudubaya a.k.a Konki Master, bado haufahamu wokovi hivyo suala la kuokoka kwake litakuwa gumu.

Akizungumza na Mwanaspoti hivi karibuni wakati wa msiba wa baba wa AliKiba, Chid amesema: “Mimi sijaokoka bwana wewe, nitaokokaje wakati hata wokovu wenyewe siujui.

Kipindi kile watu walisema nimeokoka kwa sababu waliniona kanisani ambako, kulikuwa kuna wabunge na viongozi wengine.

Sasa nawezaje kukataa wakati nimealikwa tena ilikuwa ni bahati ilikuwa siku yangu ya kuzaliwa,” Chid ambaye amekuwa akipambana kujiondoa kwenye wimbi la kutumia dawa za kulevya.

Hata hivyo, Chid ameliambia Mwanaspoti kuwa kwa sasa ameacha kutumia dawa za kulevya, lakini anashangaa baadhi ya watu kuendelea kumchukua kama mtu anayeendelea kutumia.