Cheki mikoba ya LeBron RBA

Muktasari:

  • Nyota hao wanapewa presha na Erick Kahangwa wa ABC ambaye anawafuatia kwa kufunga pointi tatu mara 10.

KAMA ni shabiki wa mpira wa kikapu, bila shaka unavutiwa na kiwango cha nyota wa Los Angeles Lakers inayoshiriki Ligi ya Kikapu Marekani (NBA), LeBron James hasa pale anapokuwa akifunga mipira ya pointi tatu.

Sasa buana Kibongo bongo katika Ligi ya Mkoa wa Dar es Salaam (RBA) kuna nyota wameanza ‘kunusa’ kiwango cha Mmarekani huyo katika kufunga pointi tatu.

Erick Lugola wa Oilers na Baraka Sadiki wa JKT wanachuana kufunga pointi tatu katika RBA, kila mmoja akiwa amefunga mara 15.

Nyota hao wanapewa presha na Erick Kahangwa wa ABC ambaye anawafuatia kwa kufunga pointi tatu mara 10.

Ukiachana na rekodi hiyo, kigogo Pazi amechapika mbele ya timu chipukizi ya Magnet katika muendelezo wa ligi hiyo.

Pazi alikubali kipigo hicho wikiendi iliyopita kwa kufungwa pointi 64-52.

Mechi nyingine, ABC ilitoa kipigo ‘hevi’ cha pointi 87-24 kwa Jogoo wakati Oilers yenyewe ikiigaragaza Kurasini Heat pointi 69-54.