Cheki Paul Pogba anavyowajulia Mbappe, Rashford

Muktasari:

Pogba amekuwa na uwezo wa kufanya hivyo kwa sababu Kocha Solskjaer kwa sasa amempa uhuru wa kufanya anachokiweza ndani ya uwanja kama anavyofanya Didier Deschamps huko kwenye kikosi cha Les Bleus.

MANCHESTER, ENGLAND

HAPA ni kukopi na kupesti tu. Watumiaji wa vifaa kama simu na kompyuta wanaelewa, kukopi na kupesti.

Basi bana hicho ndicho wanachokifanya Paul Pogba na Marcus Rashford huko kwenye kikosi cha Manchester United.

Wanachofanya mastaa hao ni kukopi kile ambacho Pogba amekuwa akikifanya na Kylian Mbappe kwenye Timu ya Taifa ya Ufaransa na kupesti Man United kwa maana ya staili ya mabao yao yanavyofungwa.

Man United kwa sasa imerudi upya kwenye makali yake tangu timu ilipokabidhiwa kwa Ole Gunnar Solskjaer baada ya Jose Mourinho kutimuliwa kutokana na timu kufanya ovyo.

Chini ya kocha mpya, Pogba na Rashford wanaonekana kutengeneza kombinesheni matata kabisa na kutengenezeana mabao, huku staili ya mabao hayo ikiwa ni kama yaleyale Pogba anayomtengenezea Mbappe wanapokuwa Ufaransa.

Rashford sasa amefunga mabao tisa na kuasisti mara saba katika mechi 22 alizocheza kwenye Ligi Kuu England msimu huu.

Katika mechi dhidi ya Tottenham, Pogba alimpigia asisti Rashford ya bao ambalo aliwahi kumtolea asisti pia Mbappe katika fainali za Kombe la Dunia 2018 walipocheza na Croatia fainali.

Ilikuwa asisti ya staili ileile. Lakini, Pogba alipiga asisti ya aina hiyo pia katika mechi dhidi ya Leicester City, ambapo Rashford alifunga bao pekee katika mechi hiyo iliyofanyika King Power.

Pogba amekuwa na uwezo wa kufanya hivyo kwa sababu Kocha Solskjaer kwa sasa amempa uhuru wa kufanya anachokiweza ndani ya uwanja kama anavyofanya Didier Deschamps huko kwenye kikosi cha Les Bleus.