Chama amaliza kesi ya Niyonzima

Muktasari:

  • Chama alisema kucheza kwake sasa kunatokana na kujipanga kwake tangu alipowasili Simba ambapo alitaka kupigania namba na mchezaji yeyote atakayemkuta.

HAKUNA siri mashabiki wa Simba wameanza kumsahau kabisa Haruna Niyonzima kwa sababu ya mavitu ya Clatus Chama, lakini Mzambia huyo amefichua hana vita yoyote na mkongwe huyo na anamheshimu.

Akizungumza na Mwanaspoti, Chama alisema hata kama sasa anacheza mechi nyingi kuliko Niyonzima lakini hajawahi kumdharau, kwani anaheshimu kipaji kikubwa alichonacho katika soka.

“Haruna (Niyonzima) bado ni mchezaji mkubwa, anastahili kuwepo Simba, siwezi kumdharau eti kwa vile kwa sasa napata nafasi ya kucheza haya ni maamuzi ya makocha sio mimi, yeye ni mchezaji muhimu sana,” alisema Chama.

Chama alisema kucheza kwake sasa kunatokana na kujipanga kwake tangu alipowasili Simba ambapo alitaka kupigania namba na mchezaji yeyote atakayemkuta.

“Kinachonifanya nicheze sasa ni kwa vile wakati nafika hapa nilijua nitawakuta wachezaji wenzangu sasa nilijiandaa kwa ushindani wa kuwania nafasi ya kucheza lakini sio kama mimi ni bora kuliko Haruna namkubali sana ni rafiki yangu pia.”