CAF yaifungia Guinea kushiriki Afcon U17 miaka miwili

Muktasari:

Uamuzi huo wa kuifungia Guinea kwa awamu mbili kushiriki fainali za AFCON U17 umetolewa na kamati ya nidhamu ya CAF mwanzoni mwa wiki iliyopita baada ya kukutana huko Cairo, Misri.

Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limeifungia Guinea kutoshiriki Fainali za Mataifa ya Afrika kwa vijana wenye umri chini ya miaka 17 (AFCON U17) baada ya kujiridhisha kuwa nchi hiyo ilifanya udanganyifu wa umri kwa wachezaji wawili kwenye fainali hizo zilizofanyika Tanzania mwezi uliopita.

Uamuzi huo wa kuifungia Guinea kwa awamu mbili kushiriki fainali za AFCON U17 umetolewa na kamati ya nidhamu ya CAF mwanzoni mwa wiki iliyopita baada ya kukutana huko Cairo, Misri.

Wachezaji walioiponza Guinea ni Aboubacar Conte na Ahmed Tidiane Keita ambao walikatiwa rufaa na Senegal ambayo waliichapa mabao 2-1.

Rufaa ya Senegal iliambatanishwa na vielelezo vilivyoonyesha kuwa Conte na Keita walidanganya umri kwa kumiliki hati za kusafiria mbili zinazoonyesha umri tofauti.

Hati za kusafiria za kwanza kwa nyota hao walizozitumia kwenye mashindano ya vijana yaliyofanyika Japan mwaka jana, zinaonyesha kuwa walizaliwa mwaka 2001.

Hata hivyo kwenye fainali za AFCON U17 nyota hao walitumia hati za kusafiria zinazoonyesha kuwa walizaliwa mwaka 2002.

Uamuzi huo wa kuifungia Guinea kushiriki AFCON U17 umeenda sambamba na ule wa kuiondoa timu yao ya vijana wenye umri huo kwenye Fainali za Dunia zitakazofanyika Brazi, Oktoba