Bushiri atumia mbinu za kisasa kupanda ligi kuu

Muktasari:

Timu mbili kutoka kila kundi zitapanda kucheza Ligi Kuu Bara msimu ujao kutoka katika Ligi Daraja la kwanza

Dar es Salaam. KOCHA Mkuu wa Polisi Tanzania, Ally Bushiri, amesema atapambana kufa na kupona kuhakikisha anairudisha timu hiyo ligi kuu.

Bushiri ambaye kikosi chake kinaongoza  kundi B, kikiwa na  pointi 19, mbele ya  JKT  Mlale  yenye pointi 18 sawa na  Coastal Union na KMC, wakifuatiwa na Mbeya Kwanza yenye 15, Mufindi United 12, Mawenzi Market 7  na Polisi Dar ndiyo inashika mkia na pointi 2.

Amesema,  anatambua ugumu wa kundi lake, lakini atahakikisha anarudi kwa kishindo na amepanga kushinda mechi zote zinazofuata.

 “Ukiliangalia kundi letu hatujapishana pointi nyingi, kama ukifungwa au ukitoa sare tayari ushapotea, nitahakikisha nakuwa na nidhamu ya kila mechi ili kuweza kupanda na kucheza ligi kuu mwakani,” anasema kocha huyo wa zamani wa Mwadui FC.Akizungumzia mbinu ambazo anatumia katika kipindi hiki ambacho ligi imesimama, anasema anataka kuhakikisha timu yake inapata mechi nyingi za kirafiki, ili wawe na utimamu wa mwili kwani bila hivyo itawasumbua.

“Najaribu kufanya mawasiliano na baadhi ya vilabu ilikuweza kupata mechi nyingi za kirafiki, wachezaji wakikaa bila kucheza watakosa utimamu wa mwili hivyo mechi hizi zitawajenga zaidi, lakini pia nitawapamuda wa kupumzika ili wasichoke,” anasema.