Bocco awapa majukumu madogo Simba

Muktasari:

  • Timu ya Simba imefuzu  hatua ya nusu fainali Kombe la Mapinduzi ikimaliza mechi ya mwisho ya makundi jana Jumanne kwa mchezo dhidi ya Mlandege ulioisha kwa Wekundu wa Msimbazi kuibuka kwa ushindi wa bao 1-0.

Nahodha wa Simba, John Bocco amewachia jukumu wachezaji waliobaki kisiwani Unguja kwa ajili ya nusu fainali ya Kombea Mapinduzi kwamba wahakikishe wanatinga fainali na kuchukuwa ubingwa.

Bocco ameyazungumza haya wakati kikosi cha wachezaji 17 kikiondoka kurejea Dar es Salaam kwa ajili ya mechi yao ya Ligi ya Mabingwa Afrika itakayochezwa Jumamosi.

Bocco alisema anawaamini wachezaji wote waliobaki Unguja ni wapambanaji ambao wataiwezesha Simba kutwaa ubingwa wa kombe hilo. 

"Tulikuwa kama tunafanya mazoezi na Tunashukuru tumefika hatua hiyo, waliobaki ni wapambanaji ambao watatwaa ubingwa wa kombe la Mapinduzi. 

"Ni mashindano mazuri ambayo yanatuunganisha wachezaji wa Bara na Visiwani hivyo tunajifunza mambo mengi kisoka," alisema Bocco.