VIDEO: Biashara wafichua Lipuli ilivyowapa mbinu za kuwanyonga Yanga

Muktasari:

Biashara wadai waliisoma Yanga ilipocheza mechi ya nusu fainali ya Kombe la FA dhidi ya Lipuli ya Iringa waliofungwa mabao 2-0 hiyo ndio siri yake ya ushindi kwa mchezo wa jana Ijumaa walipoibuka  na ushindi wa bao 1-0.

Kocha wa Biashara Amri Said amesema waliisoma Yanga ilipocheza mechi ya nusu fainali ya Kombe la FA dhidi ya Lipuli ya Iringa waliofungwa mabao 2-0 hiyo ndio siri yake ya ushindi kwa mchezo wa jana Ijumaa walipoibuka  na ushindi wa bao 1-0.

Kocha Said alisema, “Niliisoma Yanga ilipocheza na Lipuli, inatumia mipira mirefu. Nilitoa maelekezo kwa wachezaji wangu kudhibiti mbinu yao. Inawezekana mwamuzi ana kasoro kama binadamu, lakini kwangu naona amefanya vizuri,”

Kwa matokeo hayo Biashara imefikisha pointi 40 katika msimamo wa ligi na Yanga imebaki katika nafasi ya pili ikiwa na pointi 80.

Mchezo wenyewe

Yanga ilianza mchezo kwa kasi huku ikitumia mipira mirefu kupeleka mashambulizi na mara chache Biashara ilijibu kwa kutumia viungo wa pembeni.

Dakika nane za mwanzo zilikuwa za mashambulizi kwa timu zote mbili na Biashara ilipata faida baada ya kupata bao la kwanza dakika ya tisa lililofungwa na mshambuliaji Tariq Kilakala.

Kilakala alifunga bao baada ya kupata mpira wa krosi uliopigwa na Wilfred Nkouluma na mabeki wa Yanga walizembea kumbana mfungaji wakidhani ameotea.

Yanga ilizinduka kusaka baola kusawazisha, lakini mipango ilivurugwa kutokana na hali ya uwanja kutokuwa katika kiwango bora kufuatia mvua mkubwa iliyokuwa ikinyesha.