Beki Kagera amtega Ndayiragije Stars

Muktasari:

Akizungumza na Mwanaspoti, Kyaruzi alisema ataendelea kujituma ili kutimiza lengo hilo kwani amecheza Ligi Kuu kwa takribani miaka mitano, lakini hajaweza kupata nafasi ya kucheza Taifa Stars.

BEKI wa Kati wa Kagera Sugar, Erick Kyaruzi amesema licha ya kufanya vizuri msimu huu wa Ligi Kuu, lakini kwake bado hajatimiza ndoto za kucheza timu ya taifa ‘Taifa Stars’ jambo ambalo linamumiza.

Mchezaji huyo ambaye ana uwezo wa kucheza kwa ufasaha nafasi zote za ulinzi, msimu huu amekuwa katika kiwango kizuri ambapo ameisaidia klabu yake kuwa katika nafasi ya nne wakiwa na pointi 34.

Akizungumza na Mwanaspoti, Kyaruzi alisema ataendelea kujituma ili kutimiza lengo hilo kwani amecheza Ligi Kuu kwa takribani miaka mitano, lakini hajaweza kupata nafasi ya kucheza Taifa Stars.

Alisema mafanikio ya mchezaji wa soka ni kuitwa timu ya taifa, hivyo anaona bado hajafika safari yake kisoka kutokana na kutokichezea kikosi hicho ambacho kwa sasa kipo chini ya Kocha Ettiene Ndayiragije.

“Naona kwangu bado sijakamilika kwani natamani sana kuichezea timu ya taifa, unajua mafanikio ya mchezaji siku zote ni kuitumikia nchi yake kitu ambacho nakipigania,” alisema.

Alisema siri ya kufanya vizuri kwake Ligi Kuu ni kujituma na kufuata maelekezo ya viongozi wa benchi la ufundi suala ambalo limemfanya aweze kuwa katika kiwango bora.

“Kwangu naona bado sijawa katika kile kiwango ninachotaka, lakini nitaendelea kujituma kuhakikisha natimiza malengo niliyojiwekea msimu huu wa Ligi Luu,”alisema.