Beki Azam aitwa Uarabuni

Muktasari:

 Beki David Mwantika ameshindwa kufikia makubaliano na klabu yake ya Azam ambapo wakivutana juu ya hatima yake klabuni hapo, timu hiyo ikitaka kumtoa kwa mkopo huku mwenyewe akigomea uamuzi huo.

Beki wa Azam FC David Mwantika amesema mara baada ya kumalizana na uongozi wa klabu hiyo sasa anafikiria kuanza maisha mapya nje ya Tanzania.

Mwantika ambaye bado yupo katika utata wa kuachana na klabu hiyo amesema anaendelea kupokea ofa mbalimbali za kucheza soka nje ya Tanzania.

Beki huyo wa zamani wa Prisons amesema mara baada ya kumalizana na Azam FC tayari ameshapokea ofa nzuri ya kwenda kucheza Soka Saudi Arabia.

"Ni hii corona tu inawezekana muda huu ningekuwa nimeshaondoka kuna ofa nyingi nje lakini naona nitaenda Saudi Arabia," amesema beki huyo.

"Bado tunapambana na Azam hawataki kuniachia lakini mimi sitaki kuondoka vibaya ni bora tukaachana kwa amani kila mmoja akafanye lake kuna kesho pia,wanataka kunitoa kwa mkopo kwa klabu ambayo sijakubaliana nayo.

" Nimeona sasa kwa hali ilivyo bora nitoke nje kabisa nikacheze huko kuliko kubaki hapa nimekaa nje kwa muda mrefu sasa."

Utata wa Mwantika na Azam FC ulianza siku chache kabla ya kufungwa kwa usajili wa dirisha dogo wakati Azam wakimtaka kwenda Lipuli kwa mkopo hatua ambayo aligomea.