Bayi atwaa tuzo Ujerumani

Wanariadha wa zamani kutoka Kushoto Michael Jazy, Jim Ryun, Filbert Bayi, Sebastian Coe, John Walker, Steve Cram, Nourreddine Morceli na Hicha El Guerrouj katika hafla ya utoaji tuzo za riadha

Muktasari:

Bayi alivunja rekodi ya dunia ya mbio za mita 1500 kwenye michezo ya jumuiya ya madola ya 1973 iliyofanyika New Zealand, rekodi ambayo ilidumu muda mrefu kabla ya kuvunjwa, ingawa kwenye michezo ya madola haijawahi kuvunjwa tangu alipoiweka Mtanzania huyo.

MTANZANIA Filbert Bayi ni miongoni mwa wanariadha wanane wakongwe wa dunia waliotunukiwa tuzo usiku wa kuamkia jana nchini Ujerumani.

Katika hafla hiyo iliyoandaliwa na Shirikisho la Riadha la kimataifa (IAAF) kupitia Idara ya IAAF Heritage iliwahusisha wanariadha mbalimbali waliowahi na wanaotamba duniani ambapo Bayi alipewa tuzo ya kutambua rekodi yake enzi anakimbia.

Mbali na Bayi, wanariadha wengine wakongwe waliotunukiwa tuzo ni Michael Jazy wa Ufaransa, Jim Ryun wa Marekani, Sebastian Coe wa Uingereza, John Walker wa New Zealand, Steve Cram wa Uingereza, Nourreddine Morceli wa Algeria na Hicha El Guerrouj wa Morocco.

Akizungumza na MCL Digital kutoka Monaco, Bayi alisema tuzo hizo ni heshima kwao kwani IAAF Heritage inayoongozwa na Chris Turner imetambua mchango wao katika riadha.

"Zimetolewa kwa wanariadha waliowahi kuvunja rekodi katika mbio mbili tofauti kwa wakati mmoja ambapo nilivunja rekodi ya dunia ya mbio za mita 1500 na maili moja," alisema.

Sherehe hizo ambazo mgeni rasmi alikuwa mtoto wa mfalme, Nawal Bin Mohammed Al Saud, zilihudhuriwa na wanariadha waliowahi kushiriki mbio za mita 1500 na Maili moja kutoka Kenya, Kipchoge Keino, Adi Bile wa Somalia ma Eamon Couglan wa Ireland.