Basata yaitaka Miss Utalii kufuata sheria

Muktasari:

Kwa upande wa mmoja wa waandaaji wa shindano hilo, Gidion Chipungahelo 'Chips' alisema mafunzo hayo yatasaidia baada ya kuwepo habari za kukatisha tamaa kutokana na taarifa zinazoandikwa.

BARAZA la Sanaa la Taifa (Basata) limewataka waandaaji wa Miss Utalii Tanzania kufuata taratibu za sheria kwa kutopokea rushwa kwa washiriki kwani, kufanya hivyo ni kulitia doa shindano na kuleta matatizo kwa washiriki.
Hayo yalizungumza na Afisa Sanaa Mwandamizi, Bona Masenge ambaye alimwakilisha Katibu Mtendaji wa Basata, Godfrey Ngereza kwenye mafunzo yaliyoandaliwa na Kamati ya Miss Utalii Tanzania kwa waandishi wa habari za yaliyofanyika jijini Dar es Salaam, leo Jumanne.
Bona alisema mashindano hayo yamejijengea sifa na kuitangaza nchi kimataifa, hivyo taratibu na sheria zinapaswa kufuatwa kwa waandaji pamoja na vyombo vya habari kuandika kwa usahihi.
"Unapoona mapungufu kwenye eneo fulani inabidi uangalie namna ya kuficha na kuweka heshima ya shindano hilo kwani, linaelimisha na serikali inataka kuona kupitia shindano hili tunatangaza vivutio vya utalii nchini pamoja na utamaduni wetu kwa ujumla. Kuna fursa nyingi kwa warembo kupitia shindano hilo ikiwa ni pamoja na kujiajiri na kuiletea nchi yetu sifa," alisema Bona.
Kwa upande wa mmoja wa waandaaji wa shindano hilo, Gidion Chipungahelo 'Chips' alisema mafunzo hayo yatasaidia baada ya kuwepo habari za kukatisha tamaa kutokana na taarifa zinazoandikwa.
"Semina ni kwa ajili ya kujenga na kufahamishana sheria, kanuni na taratibu za muandaaji kuanzia ngazi ya kanda mkoa na kimataifa, pia itasaidia waandishi kuandika habari za uhakika na kuwafikia wananchi," alisema Chips.