Barnaba apewa ubalozi wa riadha

Muktasari:

Mashindano hayo yanayotarajia kuanza 25 Agosti mwaka huu yatajumuisha mbio za Kilomita 20, 10, 5 kwa wavulana na wasichana na 2.5 kwa watoto

MSANII wa Bongo Fleva, Barnaba Classic amepewa ubalozi katika Mashindano ya Riadha ya Selous Marathon. Barnaba amepewa ubalozi huo kuhakikisha anatangaza mbio hizo na kuwezesha watanzania kushiriki na kutangaza vivutio mbalimbali vinavyopatikana katika Mbuga ya Selous.

Akizungumza na Mwanaspoti, Barnaba alisema anafuraha kuwa sehemu ya Mashindano hayo licha ya kwamba wasanii wapo wengi.

"Wasanii wenzangu wapo wengi lakini hawajapata fursa hii, michezo ni Afya lqkini pia ni furaha inakutanisha watu wengi, kwahiyo kuwepo hapa ni jambo kubwa kwangu," alisema.

Nae Mratibu wa Mashindano hayo, Rehema Jonas alisema mbio hizo ni kwa lengo la kuhakikisha wanatangaza utalii nchini lakini pia kuwapa wananchi somo la Afya.

"Michezo ni Afya na jambo zuri ni kujikinga kuliko kujiuguza kwahiyo tumeandaa Mashindano haya wananchi washiriki kwasababu pia watapata fursa ya kutalii," alisema. Aliongeza kwamba licha ya kuwa Mbuga hiyo kupakana na mikoa mingi, wameuchagua mkoa wa Morogoro kutokana na mkoa huo kuwa sehemu rahisi kufikika.

Mashindano hayo yanayotarajia kuanza 25 Agosti mwaka huu yatajumuisha mbio za Kilomita 20, 10, 5 kwa wavulana na wasichana na 2.5 kwa watoto