Bailly aumia hatihati kuichezea Ivory Coast fainali za Afcon2019

Muktasari:

  •  Bailly anapewa nafasi ndogo ya kupona jeraha hilo kabla ya kuanza fainali Juni 21 hadi Julai 19 nchini Misri. 

London, England. Ivory Coast huenda ikamkosa beki nyota Eric Bailly katika fainali za Kombe la Mataifa Afrika (Afcon), baada ya kuumia jana usiku katika mchezo kati ya Manchester United na Chelsea uliomalizika kwa sare 1-1.

Bailly aliumia katika mchezo huo baada ya kugongana na na mchezaji wa Chelsea, Mateo Kovacic.

Beki huyo wa kati alitolewa uwanjani kwa msaada wa madaktari na alionekana akilia kutokana na uchungu wa maumivu.

Bailly anapewa nafasi ndogo ya kupona jeraha hilo kabla ya kuanza fainali Juni 21 hadi Julai 19 nchini Misri.

Juan Mata alifunga bao kwa Man United kabla ya Marco Alonso kusawazisha na kuzifanya timu hizo kutoka sare ya bao 1-1 kwenye Uwanja wa Old Trafford.

Bailly alirejea uwanjani kwa mara ya kwanza tangu alipocheza mechi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Paris Saint-Germain Machi 6.

Kocha wa Man United, Ole Gunnar Solskjaer alimuingiza Marcos Rojo kujaza nafasi ya Bailly.