Baba ampa Samatta ruksa

TETESI zinazomhusu straika wa Aston Villa, Mbwana Samatta kutaka kutimkia Uturuki si ngeni kwa baba yake mzazi, Ali Pazi Samatta ambaye naye anaona kinachoendelea kwenye mitandao ya kijamii.

Mzee Samatta alisema, bado hajafanya mazungumzo na kijana wake juu ya tetesi zinazoongelewa kuondoka Aston Villa kwenda West Brom na Fenerbahce.

“Bado hajaniambia kwasababu nilishampa uhuru kwamba alipofikia anaweza akajisimamia nakufanya vitu vikubwa, anajitambua anataka nini katika soka,”anasema baba yake.

“Akiniambia anaondoka nitayaheshimu maamuzi yake kwani atakuwa ameyatafakari kwa kina, akisema anabaki yote sawa, vitu vikiwa vigumu sana ndio nakaa naye mezani ili kujadiliana naye tuvifanyaje, ndio maana nasema licha yakuziona tetesi nasubiri aniambie asiponiambia najua anaweza akamudu,” alisema Baba Samatta na kuongeza;

“Nimemzaa na kumlea mwenyewe namuelewa Mbwana ni waaina gani, sio mrahisi wakukata tamaa kwa kusikiliza watu wanasema nini, angekuwa hivyo asingefika hatua aliopo kwani haikuwa rahisi bado watu walikuwepo wakumtia moyo na kumkejeli.”

“Ana kauli yake inasema ‘hakuna kufeli’ hiyo imebeba uhalisia wa maisha yake, sio tu mpira bali hata katika mambo yake akiamua hiki lazima nikifanye.”