Azam hiyoo, inazidi kupaa tu

Azam FC  imeendeleza moto wake kwenye Ligi Kuu Bara baada ya leo Jumanne kuichapa Ihefu mabao 2-0 katika mchezo wa Ligi Kuu Bara uliofanyika kwenye uwanja wa Sokoine Mbeya.

Timu hiyo sasa imefikisha pointi 21  na kuzizidi timu kongwe Simba na Yanga pointi nane ingawa watani hao wa jadi wana mechi mbili mkononi

 Ikicheza kwa kiwango bora  Azam ilianza kupata bao la kwanza dakika ya  55 kupitia kwa  Ayoub Lyanga na aliyefunga kwa shuti kali akimalizia  krosi ya Prince Dube.

Azam iliendelea kuliandama lango la Ihefu na kufanikiwa kupata bao la pii lililofungwa na  Iddi Selemani'Nado'  kwa kichwa akimalizia pasi safi ya Dube.

Kipigo hicho ni kama kimemkaribisha vibaya kocha  mpya wa Ihefu ,Zubery Katwila ambaye muda mwingi wa mchezo alionekana  amesimama akiwaelekeza wachezaji wake.

Katwila alijiunga na Ihefu Juzi Jumapili akitokea Mtibwa Sugar alikodumu tangu 1999 akiwa mchezaji na baadae kupewa kazi ya ukocha.

Ihefu imeonekana kujitahidi kucheza vizuri lakini  ugeni wa ligi na uzoefu mdogo  wa wachezaji wa kikosi hicho ndio umekuwa ukiwaponza na  kupoteza michezo yao mingi.

Mapaka sasa Ihefu imecheza michezo saba, imeshinda mmoja na kupoteza sita na iko nafasi ya pili kutoka mwisho kwenye msimamo wa ligi ikiwa na pointi tatu.