Aussems: Njooni muone Sevilla ikitafuta mpira kwa tochi

Muktasari:

  • Simba wamechukua ubingwa wa Ligi Kuu Bara mara mbili mfululizo lakini na linakuwa taji lao la 20.

Dar es Salaam. Kocha wa Simba, Mbelgiji Patrick Aussems amewataka mashabiki wa timu hiyo kujitokeza kwa wingi kusherekea ubingwa wakati watakapocheza mchezo wa kirafiki wa kimataifa dhidi ya Sevilla kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kesho Alhamis.

Aussems ametoa kauli hiyo muda mfupi baada ya kikosi cha Simba kumewasili Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Dar es Salaam leo saa 06:30 mchana wakitokea Dodoma.

Aussems alisema anawaomba mashabiki wa timu hiyo wajitokeze kwa wingi ili kuendeleza furaha yao ya kuchukua ubingwa msimu huu.

"Kikubwa ambacho tunawaomba mashabiki wajitokeze kwa wingi kesho kushuhudia mchezo mzuri ambao tutauonyesha kwa kutaka kumiliki mpira muda mwingi," alisema Mbelgiji huyo.

"Tutaingia kwa kucheza soka la kuvutia ili mashabiki wetu watakajitokeza waweze kufurahia muendelezo wa furaha ya kutwaa ubingwa msimu huu kama malengo yetu yalivyokuwa mwanzo.

"Kingine natamani kuona kila mchezaji anaonesha uwezo wake ndio maana tunataka kumilika mpira muda mwingi na imani yangu kuwa huenda ukawa mwanzo wao wa kupiga hatua katika maisha kupitia mpira kuonekana katika timu nyingine,"alisema.

"Tunafahamu ukubwa na ubora wa Sevilla lakini kwetu kutakuwa na faida nyingi kutoka kwao kuliko zile dakika 90, ambazo tutacheza," alisema Aussems.

Alisema wachezaji wote nimewaruhusu waende majumbani na usiku wataripoti kambini ili kupanga mikakati ya mchezo wa kesho.