Atletico Madrid yatupa ndoano kwa Lacazette

Muktasari:

Atletico imemtupia jicho nyota huyo wa kimataifa wa Ufaransa kwenda kuziba pengo la Antoine Griezmann

Madrid, Hispania. Klabu ya Atletico Madrid iko mbioni kutuma maombi ya kutaka saini ya mshambuliaji wa Arsenal, Alexandre Lacazette.

Atletico imemtupia jicho nyota huyo wa kimataifa wa Ufaransa kwenda kuziba pengo la Antoine Griezmann.

Griezmann anatarajiwa kujiunga na Barcelona katika usajili wa majira ya kiangazi.

Kocha wa Atletico Diego Simeone ameanza mchakato wa kusaka mrithi wa Griezmann aliyekuwa kinara wa mabao katika kikosi hicho.

Mapema wiki hii Griezmann alitangaza kuondoka Atletico baada ya Barcelona baada ya kucheza kwa mafanikio.

Simeone anamuona mtu pekee wa kuziba nafasi ya Griezmann ni nyota huyo wa kimataifa wa Ufaransa.

Hata hivyo, Atletico itakuwa na kazi ngumu kupata saini ya mchezaji huyo baada ya kuonyesha kiwango bora msimu uliopita akicheza pacha na Pierre-Emerick Aubameyang.

Mchezaji huyo mwenye miaka 27, amefunga mabao 13 na kutoa pasi za mwisho mara nane katika mechi za Ligi Kuu England msimu huu.

Pia Barcelona inahusishwa na mpango wa kumsajili Lacazette katika majira ya kiangazi.