Ambulance bado tatizo kwa wachezaji Mwanza

Muktasari:

Wachezaji wawili wa Mlandizi Queens walioumia katika mchezo wa leo Ijumaa na Alliance Girls Uwanja wa Nyamagana, wamepelekwa katika Hospitali ya Mkoa wa Mwanza, Sekou Toure kwa ajili ya matibabu zaidi.

Mwanza. Bado afya za wachezaji zinaendelea kuwa katika wakati mgumu kutokana na kucheza bila ya kuwapo kwa gari la wagonjwa 'Ambulance' viwanjani.


Mara kadhaa tumeshuhudia matukio hayo yakijitokeza wakati wa mechi za Ligi Kuu ya Wanaume. Leo Ijumaa limetokea tena tatizo hilo katika Uwanja wa Nyamagana baada ya wachezaji wawili wa Mlandizi Queens kuumia na kuanza kutahabika bila msaada.


Kipa Tausi Swalehe na Beki Wema Richard wameumia wakati mchezo wa Ligi Kuu ya Wanawake ukiendelea dhidi ya Alliance Girls lakini huduma ya upatikanaji wa gari ilikuwa tatizo.


Awali ilifikia hatua ya kuchukua Tax kuwapeleka hospitalini, lakini baadaye Ambulance ilifika. Iliwashusha wachezaji hao kwenye Tax kisha kuwapandisha kwenye gari hilo la wagonjwa.

Wachezaji hao wamepelekwa hospitalini ya Mkoa wa Mwanza, Sekou Toure kwa ajili ya matibabu zaidi.