Ambokile ishu ni kibali tu

Muktasari:

  • Ambokile alisema kutokucheza kwake hakumkatishi tamaa na wala hakumfanyi atamani kurudi Tanzania kwani anaamini kila kitu kitaenda sawa na kuanza kuitumikia timu yake hiyo.

STRAIKA wa zamani wa Mbeya City anayekipiga Black Leopards ya Afrika Kusini, Eliud Ambokile amefunguka sababu ya kushindwa kuanza kuitumikia timu hiyo, akidai tatizo ni kukosa kibali cha kufanyia kazi.

Ambokile alitua Leopards kupitia dirisha dogo la usajili kwa mkataba wa miezi mitatu baada ya kocha wa timu hiyo kujiridhisha uwezo alionao katika soka.

Ambokile alisema kutokucheza kwake hakumkatishi tamaa na wala hakumfanyi atamani kurudi Tanzania kwani anaamini kila kitu kitaenda sawa na kuanza kuitumikia timu yake hiyo.

“Nilipewa mkataba wa miezi mitatu unaomalizika Juni mwaka huu, nitasalia hapa kwa namna yoyote kwani naangaliwa mazoezini na makocha wameridhika na uwezo wangu, ila siwezi kucheza kwa vile sina kibali cha kazi.”

Akizungumzia maisha ya Sauzi, Ambokile alisema anayafurahia kwani hali ya hewa haijapishana sana na Mbeya na kuhusiana na vyakula pia anaweka wazi kuwa havimpi changamoto kwa sababu vyakula vingi havina utofauti na alivyokuwa anakula.