Alliance, Malale kila mtu kivyake

Muktasari:

Malale Hamsini aliisaidia Alliance kubaki Ligi Kuu msimu ujao baada ya kuchukua mikoba ya mtangulizi wake, Mbwana Makata aliyetemwa kikosini hapo kutokana na matokeo yasiyoridhisha.

Mwanza. Klabu ya Alliance ya jijini hapa imeshindwa kufikia makubaliano ya kuongeza mkataba mpya na kocha Malale Hamsini hivyo klau hiyo italazimika kuajiri kocha mwingine kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Bara.

Malale ameifundisha timu hiyo msimu uliopita akichukuwa nafasi ya Mbwana Makatta aliyetupiwa virago baada ya kupata matokeo mabovu mfululizo.

Afisa Habari wa klabu huyo, Jackson Mwafulango alisema uongozi utatangaza benchi jipya la ufundi mapema wiki hii ingawa habari za ndani kutoka klabu hiyo zinasema aliyekuwa kocha wa Stand United, Athuman Bilali 'Bilo' atakuwa miongoni mwa wataalamu wa benchi hilo.

“Tulihitaji sana huduma ya Malale lakini tumeshindwa kuafikiana kutokana na pande zote kuwa na hoja zake za msingi, hivyo tunamtakia kila la heri na tutaendelea kutambua na kuheshimu kazi yake,” alisema Mwafulango.

Malale alisema kuna mambo ambayo hayajafikia makubaliano hivyo kulazimika kutoongeza mkataba mpya na sasa yupo huru.

“Hadi sasa nipo huru na timu itakayohitaji huduma yangu niko tayari mkataba wangu ulimalizika tangu Mei 30, kuna mambo tumeshindwa kukubaliana hivyo kila pande imeridhia kutoongeza mkataba mpya," alisema Malale