Alichosema Maxime baada ya kuichapa Simba nje, ndani

Muktasari:

Kocha Mkuu wa Simba alifanya mabadiliko katika mchezo wao na Kagera Sugar kwa kumtoa Mghana James Kotei na kumwingiza Jonas Mkude. Pia, aliwatoa, Mohammed Ibrahim na Hassan Dilunga na kuwaingiza Clatous Chama na Rashid Juma.

Dar es Salaam. Baada ya Kagera Sugar kuifunga Simba bao 1-0, Kocha Mkuu wa Kagera Sugar, Mecky Maxime amesema riziki yao imetolewa na Mungu.

Kagera Sugar ilipata bao la kuongoza na la ushindi baada ya beki wa Simba, Mohammed Hussein 'Tshabalala' kujifunga katika dakika ya 41.

Akizungumza baada ya mchezo huo, Maxime alianza kwa kusema riziki siku zote hutolewa na Mwenyezi Mungu.

"Niliwaambia wachezaji wangu twendeni tukacheze tukiamini Mungu yupo kwani ukiingalia Simba ni timu nzuri,"alisema Maxime kocha na mchezaji wa zamani wa Mtibwa Sugar.

Alisema, walikuwa na mipango katika mchezo huo kwani walijua simba ni timu bora na kuuliza:

"Goli mmeliona, tumezawadiwa." "Katika mchezo huu sisi tulichokuwa tunafanya ni kuwashtukiza Simba ambao walikosa njia mbadala ya kutufunga,"alifafanua Maxime.