Aishi Manula asherehekea birthday ndani ya ndege!

Muktasari:

  • Aishi amesafiri pamoja na wachezaji wenzake kwa ajili ya mchezo wao dhidi ya Ndanda FC utakaopigwa Uwanja wa Nangwanda.

Dar es Salaam. Nyota  wa Simba na Taifa Stars, Aishi Manula leo Alhamisi anasherehekea siku yake ya kuzaliwa 'birthday' akiwa ndani ya ndege ya Precision kwenda mkoani Mtwara.

Aishi amesafiri pamoja na wachezaji wenzake kwa ajili ya mchezo wao dhidi ya Ndanda FC utakaopigwa Uwanja wa Nangwanda.

Imemfanya siku yake hiyo ya kuzaliwa iwe ya baraka kwake sawa na mlinda mwenzake Aleksandr Belenov wa Ufa ya Ligi Kuu  Russia.

Manula ambaye ni sehemu ya wachezaji wa Simba waliosafiri leo kwenda Mtwara kwa ajili ya mchezo wao wa tatu wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Ndanda.

Ametimiza miaka 23, huku kwa Belenov akiwa na  miaka 32, ambapo Manula alizaliwa 1995, mkoani Morogoro alikuwa na kuanza maisha yake ya soka kabla ya kujiunga na Azam.

Akiwa na Azam, aliisaidia kutwaa mataji kadhaa ikiwemo lile la Ligi Kuu Bara kwa mara ya kwanza msimu wa 2013- 2014.

Kipa huyo anayefanya vizuri sasa akifuata nyayo za Juma Kaseja wa KMC ambaye alitawala kwenye anga hizo kwa zaidi ya miaka 10 akiwa namba moja kutokana na kufanya kwake vizuri.

Ameanza msimu huu kwa kasi baada ya kuidakia Taifa Stars mechi ya kufuzu AFCON dhidi ya Uganda wakatoka suluhu, pia ameichezea klabu yake ya Simba katika mechi mbili za ligi kuu dhidi ya Tanzania Prisons na Mbeya City  akatoka kabla ya dakika 90 kwa sababu ya maumivu.

Nyota wengine waliozaliwa na Aishi Manula ni washambuliaji  Thomas Müller (29)  wa Bayern Munich ya Ujeruman na Fraizer Campbell (31) aliyewahi kuichezea Manchester United ya England.